Tuesday, 21 May 2013

Kumekucha Usajili, Ngassa atua rasmi Yanga


 


Posted  Jumanne,Mei21  2013  saa 10:15 AM
In Summary
  • Yanga imemtambulisha rasmi Mrisho Ngassa aliyesaini mkataba wa miaka miwili huku ikisisitiza kuwa bado mapambano yanaendelea kusaka mastaa wa kusuka kikosi cha Afrika.
KAMA Mwanaspoti ya Januari 26 mwaka huu ilivyokuwa ya kwanza kufichua, jana Jumatatu, Yanga imemtambulisha rasmi Mrisho Ngassa aliyesaini mkataba wa miaka miwili huku ikisisitiza kuwa bado mapambano yanaendelea kusaka mastaa wa kusuka kikosi cha Afrika.
Mwenyekiti wa Kamati ya Uchumi na Fedha ya Yanga, Ridhiwani Kikwete baada ya kutambulishwa Ngassa aliandika kwenye ukurasa wake wa Facebook; "Mambo yameanza ndani ya Jangwani, mtani usione wivu natengeneza timu ya Afrika." Maneno hayo yakiwa ni kuikejeli Simba baada ya kuwapora Ngassa.
Jopo la Yanga likiongozwa na Mwenyekiti wa usajili pamoja na kamati ya mashindano, Abdallah Bin Kleb jana, Jumatatu walikubaliana kuwa watafanya usajili wa aina yake ingawa hakutakuwa na mabadiliko makubwa sana kikosini kwavile timu iliyochukua ubingwa ni imara.
Bin Kleb ambaye alifanikisha usajili wa Mbuyu Twite, Haruna Niyonzima na Kelvin Yondani alisisitiza kwamba mambo yanakwenda kimyakimya na watapata wachezaji wote wanaowahitaji kwavile kocha ameshawaambia mahitaji yake kwa Ligi ya Mabingwa msimu ujao.
Alipoulizwa kuhusu Shomari Kapombe ambaye mkataba wake na Simba unamalizika Desemba, Bin Kleb alicheka na kusema wanafanya mambo yao kimyakimya na wataweka hadharani kimoja baada ya kingine kila kinapokuwa tayari huku akisisitiza kwamba wana malengo makubwa msimu ujao.
Alisema hawezi kuweka hadharani silaha zake kwavile Simba wanaweza kutibua na kwamba suala la Haruna Niyonzima 'Fabregas' kusaini mkataba mpya Yanga litakamilika wiki hii: "Nakuhakikishia Niyonzima haendi kokote si Simba wala Azam, wanajihangaisha tu."
Ngassa alitua Jangwani kwenye makao makuu ya Yanga majira ya saa nne asubuhi jana Ijumaa akiambatana na Bin Kleb, Mjumbe wa kamati ya Usajili, Seif Magari, Francis Kifukwe ambaye ni Mjumbe Bodi ya Udhamini, Kaimu Katibu Mkuu, Lawrence Mwalusako na Mussa Katabaro ambaye ni Mjumbe Kamati ya Utendaji.
Ngassa ambaye wiki chache zilizopita aliwaambia viongozi wa Simba wampe fungu asaini mkataba mpya alisema jana kuwa: "Nimerudi kwenye klabu yangu ya zamani, kweli naipenda Yanga kwa mapenzi ya dhati na nitaitumikia kwa nguvu zote. Nilipoingia Simba watu walikuwa na woga na mimi kutokana na tetesi kuwa nina mapenzi na Yanga lakini kama mchezaji nafahamu majukumu yangu na nikaitumikia kwa nguvu zote."
"Na sasa ndiyo nimerejea nyumbani rasmi. Nawashukuru mashabiki wote. Nilienda Simba kwa mkopo nikitokea Azam FC na sasa ni mchezaji huru nimemaliza mkataba, suala la kuwa nina mkataba na Simba ni maneno tu, sijasaini mkataba wowote na Simba,"alifafanua Ngassa na kusema pesa na gari aina ya Verossa alipewa na Simba ili kumshawishi baada ya awali kukataa.
Bin Kleb alidakia kuwa: "Tumemrudisha Ngassa nyumbani na tunamkaribisha kwa nguvu zote maana alikwenda timu nyingine kutafuta riziki tu, nampongeza kwa kuonyesha uaminifu kwa Simba kwavile tuliongea naye mapema kama miezi sita au mitano lakini naye alionyesha uwezo wake uwanjani na uaminifu Simba."
"Hata mechi ya juzi alijitoa kwa kucheza kiwango cha juu na penalti alisababisha yeye, (penalti hiyo alipiga, Mussa Mudde raia wa Uganda akakosa) ni uaminifu," alisistiza Bin Kleb na kuthibitisha mchezaji huyo amesaini mkataba wa miaka miwili.
Mwenyekiti wa Kamati ya usajili ya Simba, Zakaria Hanspope alisema: "Sisi tunaishangaa Yanga. Ngassa ni mchezaji wetu, ana mkataba wa mwaka mmoja. Tulimchukua Azam kwa mkopo wa mwaka moja, na tukamsaininisha mkataba mwingine wa mwaka mmoja kwa ajili ya kuitumikia Simba."

No comments: