Wednesday, 22 May 2013

Kasoro hizi Tuzo za Kili mpaka lini?

 

Msanii akishiriki vilivyo jukwaani 

Tuzo za muziki za Kilimanjaro (Kili Music Awards), zimekuwa zikifanyika mfululizo tangu mwaka 2000. Ndizo tuzo kubwa na pekee kwa aina yake katika kuenzi na kuthamini mchango wa wasanii katika ustawi wa muziki nchini.
Mwaka huu, tuzo hizo zinazodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia Bia ya Kilimanjaro, zimepangwa kufanyika Juni 8, jijini Dar es Salaam.
Tuzo hizi zinazosimamiwa na Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa muziki, kwa kiasi kikubwa zimefanikiwa kuleta mageuzi katika fani ya muziki.
Hata hivyo, katika kipindi chote cha kufanyika kwake, yaani kwa mwaka mara moja, changamoto nyingi na malalamiko yamekuwa kiini kinachotia dosari ubora wa tuzo hizo.
Malalamiko yanayofanana kila mwaka kutoka kwa wasanii na wadau wengine wa muziki dhidi ya waandaaji wa tuzo hizo, kumewafanya baadhi kuzivisha taswira ya ubabaishaji.
Wengine wamefikia hata kuzitafsiri kama ‘mradi’ wa wachache uliokosa tija katika ustawi wa muziki wa Tanzania, jambo ambalo halikuwa kiini cha kuanzishwa kwake.
Mara kadhaa wasanii wamekuwa wakizisusia hata pale majina yao yanapojumuishwa kuwa ni tuzo, wengine wakilalamika mfumo mbovu wa kuwateua wasanii wa kuingia kwenye kinyang’anyiro hicho.
Wasanii wengi wanalalamika utaratibu wa uteuzi kwa washiriki wa tuzo hizo, huku baadhi wakisema umejaa upendeleo na wengine wakisema haujawekwa wazi kwa wasanii.
Kukosea kwa uwazi unaolezwa na wadau na wasanii pengine ndiko kunakosababisha malalamiko kuibuka kila mwaka, jambo ambalo linaleta mitazamo tofauti.
Ni vigumu wasanii kujua kwa nini hakuteuliwa au kwa nini msanii fulani kateuliwa kama hakuna mfumo ulio wazi na kutambulika kwa wasanii ambao ndiyo waelekezwa wa tuzo hizo.
Pengine ni kweli kwamba, siyo malalamiko yote kutoka kwa wadau na wasanii wa muziki yanaweza kuwa na msingi, lakini swali la kujiuliza kwa nini malalamiko yawe hayo hayo kila mwaka.
Tunadhani ipo sababu kwa wandaaji kuyatupia macho malalamiko hayo ili kujenga msingi wa imani ambayo tangu mwaka 2000 imekuwa ikilalamikiwa na wasanii.

No comments: